Thursday, November 6, 2014

WATALII WALALAMIKIA RUSHWA KATIKA VIZUIZI VYA BARABARANI HUKO ZANZIBAR.




KAMA vituo 66 vya treni havitoshi katika safari nzima ya utalii, Teresa Williamson wa  Australia na Annemarie Schuller wa Uholanzi wamesema Watanzania wanaishi katika mazingira magumu na wanastahili kubadilika.
 Kauli hiyo wameitoa wakati wakizungumza na Mwandishi wa makala haya muda mfupi kabla ya kuondoka kurejea makwao baada ya ziara ya wiki mbili katika maeneo mbalimbali nchini.
Katika ziara yao ya kitalii walitumia treni, barabara na maji tena kwa kutumia jahazi wakitokea Pangani Tanga hadi Zanzibar.
Nilitaka kujua baada ya utalii wao wameona nini nchini Tanzania walisema pamoja na kufanikiwa kuwaona wanyama wakubwa watano kama walivyofikiria wakati wakiwa makwao wameshuhudia maisha masikini zaidi kuliko matarajio.
“Sijui inatokeaje watu wengi wana simu za mkono lakini ukiangalia maisha yao unayaona kuwa magumu sana,” alisema Teresa ambaye alifafanua kwamba ugumu wa maisha unaonekana katika miundombinu na usafirishaji, ulaji na utunzaji wa mazingira.
Wakiwa wamezaliwa mjini hawakuwa wanajua vijijini kukoje mpaka walipofika nchini Tanzania na kukumbana na hali ambayo hawakuitarajia  hata kidogo.
Pamoja na kushuhudia matukio yasiyokuwa ya kawaida katika safari na mbugani ugumu wa maisha ambao wao wataendelea kuangalia ni mawasiliano, usafirishaji, na usalama.
Wamesema katika safari yao wamekumbana na tatizo  kubwa la chakula, usahihi wa taarifa na tatizo la mawasiliano.
“Pamoja na wananchi kuwa marafiki tumeona tatizo kubwa la usafiri na aina ya chakula kinacholiwa na usafi,” alisema Schuller ambaye kitaalamu ni mganga wa meno.
Kwa mtazamo wa watalii hao taifa hili linahitaji kubadili wananchi wake kwa kuwapa elimu ya kutosha kuhusu mazingira yanayowazunguka hasa kwa kujali aina ya mlo wanaokula, usafi wa mazingira na kujali gharama kwa huduma wanazotoa kwa wageni.
Teresa alisema kwa kuwa na aina moja ya chakula Ugali na wali muda wote bila maziwa mboga za majini kunatengeneza aina ya udumavu ambao unachochea watu kukosa lishe bora.
“Tumekuwa tukikumbana na chakula cha aina ile ile kila mahali tunapoenda, chakula cha nafaka ambacho ni wanga lakini hukutani na matunda, mboga za kijani na maziwa,” alisema Teresa.
Pamoja na kuzungumzia mlo, wageni hao walizungumzia  tatizo la rushwa na kusema walipokuwa Zanzibar pamoja na kuhisi kwamba ulinzi ni mkali kutokana na kusimamishwa kila mara katika gari, lakini waliona kuna kitu si sahihi wakati wa mazungumzo kati ya dereva na askari.
“Pale tuliona shida kidogo kwanini wanapenyeza mkono tena unaona kwa uangalifu mkubwa?” Alisema  Annemarie ambaye alisema matendo waliyokumbana nayo yanatia wasiwasi hasa unaposimamishwa mara saba katika kipindi cha dakika 40 wakati wakiwa kisiwa cha Zanzibar.
Kwao wanaamini kwamba lipo tatizo la rushwa na pia tatizo la lugha kwani wengi wameshindwa kuwasiliana nao kutokana na shida ya lugha kiasi ya kwamba wapo watu walikuwa wanawakwepa kwa sababu hawaelewani na wakati mwingine walifanya maamuzi ambayo hayakuwa sahihi kutokana na lugha gongana.
Anasema walipofika Tanga waliambiwa wanaweza kufika Zanzibar kupitia Pangani.Walisema usafiri uliwachosha na hata walipofika Pangani wakagundua kwamba mawasiliano si sahihi lakini wakaingia katika boti na kuelekea Zanzibar.
Boti hiyo ambayo ilikuwa kila mara inatolewa maji, iliwaogopesha sana lakini hata walipokuwa wakitaka kujua wanajiokoaje walijikuta wakiambulia kuambiwa kwamba njia za kujiokolea ni palepale walipo.
Hata hivyo walifarijika baada ya kugundua maboya ya kujiokolea ndio waliyoyakalia.
Pamoja na kufurahishwa na matembezi yao hasa kwa kuona kwamba wameweza kuwaona wanyama wakubwa kama tembo, chui, simba, faru,twiga na nyati walisema ipo haja ya kupunguzwa kwa kiingilio kwani kwa sasa wanakiona kama ghali.
Nilipomuuliza kuhusu Serengeti kama itakufa, alisema kwamba hadhani kwani anaona kwamba bado haijavurugwa sana na kama Watanzania watakubali kwamba ile ni mali yao haitakufa.
“Ni suala la kuelimika na kuhakikisha kwamba utamaduni unajali mazingira, unajali afya na wajibu,” alisema Teresa ambaye katika miaka yake 55 alisema Afrika bado ni bara la kutembelea.
Alisema walifika Sumve kuwaona jamaa zao na marafiki, lakini walishangazwa na wingi wa vituo ambapo treni inasimama japo waliona kwamba hali ile inaweza kuwa inasaidia mzunguko sahihi wa uchumi  wa eneo hilo.
“Njiani tuliona mengi lakini nadhani baya kabisa ni watu kutokujali mazingira yao. Uchafu unatupwa kila mahali na hata maeneo mengine hayakuwa na vyoo na yale yaliyokuwa na vyoo hata karatasi laini za chooni zilikosekana,” alisema Teresa.
Kwa maneno yao watu wanatakiwa kubadilika kupitia elimu ili kutambua kwamba kuna haja ya kuwa na mazingira safi kwa manufaa yao na kizazi kijacho.
“Unakosaje mahali pa kujisaidia? Umelipa fedha ili ufurahi inakuaje unapokosa huduma,” aliuliza Teresa.
Kwa maneno yao wenyewe ugumu wa kupata huduma inayoridhisha kwa fedha halisi  si tu katika maeneo waliyofikia bali hata katika usafiri.
“Ukiwa peke yako huwezi kufanikiwa,” alisema Teresa na kuungwa mkono na Annemarie ambaye yeye kuja Afrika ilikuwa mara yake ya kwanza. Moja ya tatizo ni kukosekana kwa uaminifu miongoni mwa watu wanaoandaa usafiri ambao wamekuwa wakiwatoza ada kubwa kuliko wanayokuja kujua baadaye.
Yalikuwa ni maoni ya mwandishi wa makala haya kwamba tatizo hilo linatokana na kutumia wakala katika masuala ya utalii na badala yake watu  ambao wamejitangaza kujua Tanzania na kwamba watawapokea.
Watu hao ambao unaweza kulinganisha na vishoka wanachojali wao ni kuongeza cha juu na kuwafikisha watalii wao katika maeneo ambayo ni rahisi na wakati mwingine bila kuwa na muunganisho mwema.
Pamoja na udhaifu katika masuala ya utalii hasa mawasiliano na upashanaji wa taarifa elimu inayotakiwa miongoni mwa wananchi ni kubadili masuala yao yanayowafanya wawe na maisha magumu.
Kwa watalii hao wamesema hawajawahi kuona ardhi yenye rutuba kubwa kama Tanzania na kinachotakiwa kufanywa ni watu wake kutumia fursa zilizopo kujikwamua katika dhiki ya umasikini na kuboresha maisha yao.
Walielezea kufurahishwa na ukarimu uliofanywa na Wapare walipoenda kutembelea eneo la Mbagha ambako walilala Tona Lodge na kupata maelezo kuhusu kijiji na kutembelea vivutio mbalimbali likiwemo jiwe lililotumika kuua watoto waliokuwa wanafikiriwa wana mikosi.
Naam, mpaka mwisho wa mazungumzo wageni hao walilalamikia usafi, utunzaji wa mazingira, mfumo wa lishe na mawasiliano hafifu pamoja na lugha gongana unaleta utata wa uaminifu.

Sunday, June 16, 2013

DK. HOSSEAH WA TAKUKURU AFUNGUKA, ASEMA TAKUKURU INATENGWA NA SERIKALI.



Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah 

Dodoma. Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah, amefunguka na kueleza sababu za taasisi yake kushindwa kuwakamata walarushwa wakubwa kwa kuwa Serikali imemfunga mikono.
Akitoa majumuisho katika Mkutano Mkuu wa Chama cha Wabunge Wanaopambana na Rushwa nchini (APNAC) jana, Dk Hoseah alisema kuwa Serikali imeitenga Takukuru na kuwafanya waishi kama yatima.
Huku akishangiliwa na idadi kubwa ya wabunge, mkurugenzi huyo alisema kuwa amekuwa akishangazwa na lawama ambazo amekuwa akibebeshwa kila wakati kuwa ameshindwa kumaliza rushwa wakati bila kuziangalia sheria.
“Mnanipa lawama kila wakati, lakini huwezi kuanzisha chombo kama Takukuru halafu ukamfunga mikono mhusika, na mimi mmenifunga mikono nifanyeje jamani? Alihoji na kuongeza:
“Hata katika rasimu ya Katiba bado mmetutenga kama watoto yatima, wenzetu wote mmewaweka tena hata CAG mmesema kuwa mamlaka yake akiteuliwa basi asiingiliwe wala kuhojiwa…mamlaka gani mtu asihojiwe jamani, mimi nikiuliza Takukuru mnasema subirini Serikali ya Tanganyika.”
Gazeti la Guardian la Uingereza la Jumapili ya Desemba 19, 2010, lilitoa taarifa ya siri kuhusu wala rushwa wakubwa kulindwa Tanzania. Gazeti hilo lilichapisha taarifa za mtandao wa WikiLeaks uliokuwa ukimilikiwa na mwandishi wa habari wa Australia, Julian Paul Assange, ukimnukuu Dk Hoseah.
Dk Hoseah alinukuliwa na WikiLeaks akimueleza mwanadiplomasia wa Marekani aitwaye Purnell Delly, Julai 14 jijini Dar es Salaam mwaka 2007 kuhusu uwezo na nia ya Rais Kikwete katika kushughulikia ufisadi.
Alidai Rais Jakaya Kikwete alikuwa anakwamisha kuchunguzwa kwa vigogo wa Serikali wanaotuhumiwa kwa vitendo vya rushwa, na pia anahofia maisha yake kama mkuu wa Takukuru. Hata hivyo, Dk Hoseah kwanza alikiri kukutana na ofisa huyo ofisini kwake Julai 2007, lakini alikanusha kuzungumza kuwa Rais Kikwete alikuwa hataki sheria ichukue mkondo wake katika kuwachunguza vigogo wanaotuhumiwa kwa rushwa.
Atoa ushauri kwa Serikali
Kwa mara ya kwanza jana kiongozi huyo aliitolea uvivu Serikali kuwa imekuwa ikichangia mambo mengi katika rushwa ikiwamo usiri mkubwa katika rasilimali za nchi.
“Lazima Serikali iwe wazi, huwezi kuwaficha wananchi rasilimali zao eti ni siri kwa sababu ya sera mbovu, tunawaambia wananchi watanufaika na mirabaha ya asilimia tatu hiyo siyo sahihi jamani ndiyo maana tunashindwa kutoa majibu kwa wananchi wetu hilo ni tatizo jingine linalosababisha mambo ya rushwa,”alisema na kuongeza: “Siyo kila jambo ambalo serikali inapewa ushauri ni baya.”
Alipinga kitendo cha viongozi kuwa na kigugumizi katika uwajibikaji na akataka itungwe sheria kali ya kutaka kiongozi awajibike mara anapokuwa ametuhumiwa kwa jambo lolote aachie ngazi na kupisha uchunguzi kama ilivyo kwa nchi zingine.
Credits; Gazeti la Mwananchi

ELIMU YA NAMNA YA KUEPUKA RUSHWA KWA SEKTA YA AFYA WILAYANI NACHINGWEA.

 Wadau wa Afya toka maeneo mbalimbali ya Nachingwea walikutana katika Ukumbi wa TRC mjini Nachingwea na moja ya somo walilofundishwa ni Mapambano dhidi ya Rushwa.

Wanafunzi Chuo cha UUguzi Nachingwea wakipata elimu ya Mapambano dhidi ya Rushwa toka kwa Maafisa wa TAKUKURU waliowatembelea hivi karibuni.

ELIMU YA MAPAMBANO DHIDI YA RUSHWA YATOLEWA KWA WANAFUNZI WA SEKONDARI WILAYANI NACHINGWEA.

 

Afisa wa TAKUKURU Bw. Hassan Omari wa Nachingwea akipokea risala toka kwa kiongozi wa Klabu ya Wapinga wa Rushwa shule ya sekondari Marambo wakati wa ziara ya uhamasishaji wa mapambano dhidi ya rushwa hivi karibuni.

Baadhi ya wanafunzi shule ya sekondari Marambo huko Nachingwea wakisikiliza mawaidha toka kwa maafisa wa TAKUKURU(hawapo pichani).

Wednesday, November 14, 2012

MBOWE KUIFUTA TAKUKURU MARA AKIINGIA MADARAKANI.

MBOWE ASEMA CHADEMA IKICHUKUA MADARAKA ITATIMUA WATENDAJI WOTE WA TAKUKURU KWA VILE WAMESHINDWA KUZUIA RUSHWA CCM.


Mwenyekiti wa chadema,Freeman Mbowe akiwa na keki aliyokabidhiwa na wakulima wa ngano Babati,ambao walimuomba awasaidie kutetea kurejeshwa mashamba ya Ngano yaliyokuwa na shirika la chakula la Taifa(NAFCO) ambayo sasa yamebinafsishwa na hayaendelezwi. Kulia ni   diwani wa viti maalum Hanang, Sara Joseph

Mwandishi wetu, Hanang’
MWENYEKITI wa Chadema, Freeman Mbowe amependekeza kuvunjwa kwa Taasisi za Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kwani badala ya kupambana nayo inaipalilia.
Akifungua tawi ya Chadema Kata za Katesh linalopakana na ofisi za Takukuru Wilaya ya Hanang, Mkoa wa Manyara juzi, Mbowe alisema taasisi hiyo imeshindwa kazi.


Mbowe alisema Takukuru imeshindwa kudhibiti hata rushwa ya wazi ndani ya CCM kwenye chaguzi ambazo zilifanyika hivi karibuni.
“Hakuna ambaye hakujua rushwa ndani na CCM na jinsi ambavyo imeathiri chama hicho, lakini Takukuru wameshindwa kupambana na rushwa hiyo badala yake wanailea,” alisema Mbowe.


Alisema Rais Jakaya Kikwete ambaye anasimamia Takukuru iliyopo kwenye wizara yake, ameshindwa kuibana ndiyo sababu hata yeye amekuwa akilalamika.
Pia, Mbowe alifungua matawi kata za Endasaki na Ganana, alisema kutokana na Takukuru kushindwa kupambana na rushwa, isipovunjwa chama hicho kikiingia madarakani kitawatimua watendaji wote wa taasisi hiyo ili wafanye kazi nyingine.


Alisema Takukuru imeshindwa hata kusaidia kurejesha mabilioni ya fedha za Watanzania ambayo yamefichwa nchini Uswis.


“Hawa Takukuru walipaswa kuanza kufanya uchunguzi juu ya fedha hizo baada ya kupata taarifa na kusaidia taifa kuzipata, lakini wamekaa kimya,” alisema Mbowe.


Alisema kutokana na ukimya huo, ndiyo sababu Chadema kupitia Naibu Katibu Mkuu wake, Kabwe Zitto waliomba serikali kufanya uchunguzi na kutoa taarifa bungeni juu ya walioficha fedha na utaratibu wa kuzirejesha.


“Bunge lijalo, kama wasipoleta taarifa ya maana juu ya fedha za Uswis tunajua la kufanya, nadhani mmeona jinsi hoja hii ilivyoungwa mkono na watu wengi,”alisema Mbowe.


Awali, Mbowe alizitaka ofisi hizo za Chadema, alizofungua kuwa kimbilio la wanyonge kutoa kero zao na kusaidiwa badala ya kuwa maeneo ya kukaa viongozi pekee.
Chanzo. Gazeti la Mwananchi

Sunday, November 4, 2012

MBUNGE ZUNGU WA ILALA AKAMATWA KWA RUSHWA

 

Mbunge Zungu wa Ilala Anaswa Akitoa Rushwa

NewsImages/6661242.jpg
Mbunge wa Ilala, Musa Zungu
Watu watano akiwemo mbunge wa Ilala Musa Zungu wamekamatwa na Taasisi ya kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoani Dodoma wakidaiwa kutoa rushwa kwa wajumbe wa Jumuiya ya wazazi ili wawachague.
Kamanda wa Taasisi hiyo Eunice Mmari alisema Zungu alikamatwa katika Hotel ya Golden Crown majuzi kati ya saa mbili na nusu na saa tatu usiku.

Eunice alisema baa ya taasisi yake kupata taarifa hizo walianza kumfuatilia kwa karibu mgombea huyo na ndipo walipomsikia akitoa maagizo kupitia simu ya mkononi kuagizia nani apewe kiasi gani.

Alisema baada ya hatua hiyo TAKUKURU walianza kumfatilia Zungu na ndipo waligundua kuwa yupo katika gari ndogo aina ya Toyota Mark –II huku akifuatana na gari jingine aina ya Prado ambalo ndiko fedha na wapambe wake walikuwa wamepanda.

Alisema baada ya kulisimamisha gari hilo alilokuwemo Zungu ghafla Prado hilo liliweza kutoroka na kumuacha Zungu na ndipo alipokamtwa na kuhojiwa.

Alisema hata hivyo TAKUKURU waliweza kufuatilia mitandao ya simu na kisha kubaini kuwa fedha hizo zilikuwa zikigawiwa na mmoja wa wakala wake ambaye naye kwa sasa amekamtwa.

Kamanda huyo aliwataja wengine waliokamatwa na Zungu ni pamoja na Yahya Khamis Danga , Busulo Mohamed Pazi na Famik Joseph Mang’ati.

Alisema kwa sasa watuhumiwa hao wote wameachiwa kwa dhamana huku uchunguzi zaidi ukiendelea na watafikishwa mahakamani mara baada ya kukamilika.

Aidha kamanda huyo alisema mwingine aliyekamtwa ni pamoja na Fatuma Kasenga ambaye ni mwenyekiti wa jumuiya ya Wazazi kutoka Mkoa wa Mbeya.

Alisema mwenyekiti huyo alikamatwa usiku wa kuamkia juzi, saa tisa usiku katika hoteli ya Kitoli mjini hapa akiwanunulia wajumbe wake chakula.

Kamanda huyo apia alisema kuna taarifa zaidi ambazo zinamtaja Alhaji Abdalah Bulembo kuwa naye amekuwa akitajwa sana katika utoaji huo wa rushwa.

Alisema hata hivyo wanaendelea na uchunguzi dhidi ya tuhuma za Bulembo na wamepata taarifa za awali kuwa anatoa rushwa hizo nyumbani.

Tuesday, September 25, 2012

HAKIMU WA ILALA ASOMEWA MASHTAKA YA RUSHWA KISUTU.

Hakimu na Rushwa                                                                    

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala Pamela Kalala (kushoto),akitoka katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam jana,baada ya kusomewa shitaka la kuomba rushwa ya Shilingi milioni tatu.Picha na Michael Matemanga