Tuesday, August 21, 2012

MKOMBOZI WA TANZANIA TOKA MAKUCHA YA RUSHWA NI MTANZANIA MWENYEWE.

 Nani ataikomboa Tanzania kwenye makucha ya rushwa?

Jenerali Ulimwengu.
HATA kwenye maandiko ya vitabu vitakatifu tunaambiwa kuwa, Mwenyezi Mungu baada ya uumbaji wa dunia alimweka Adamu na Hawa katika Bustani ya Edeni na kuwapa uhuru wa kula matunda yote katika  bustani ile isipokuwa matunda ya mti uliokuwepo katikati ya bustani.
Kwa wanaofuatilia maandiko ya dini wanafahamu kilichotokea. Hapa nchini kuna sheria na maneno mengi yanayowataka viongozi na raia wa kawaida kutojihusisha na vitendo vya rushwa.
Lakini ajabu ni kwamba hivi majuzi tumesikia shutuma nzito za vitendo vya rushwa zikitolewa ndani ya Bunge vikiwahusisha viongozi wa Kamati za Bunge hususan Kamati ya Nishati na Madini, Hesabu za Serikali za Mitaa na Hesabu ya Mashirika ya Umma.
Kiukweli  tunachokiona si cha ajabu, maana ni taswira ya mambo ambayo sisi kama jamii tumeyakubali, tumeyapokea na kuyafanya kuwa sehemu ya maisha yetu. Limekuwa ni jambo la kawaida mtumishi fulani kula rushwa na kujitajirisha harakaharaka na watu kumsifu kwamba eti ana akili sana!
Katika baadhi ya vitengo kama vile mahakamani, polisi, idara za ardhi au maliasili kama ambavyo iliwahi kuaninishwa na Tume ya Joseph Warioba, ulaji wa mlungula ni  tabia ambayo baada ya muda imegeuka na kuwa ‘mazoea’ na hatimaye kuwa haki.
Wanaofanya hivyo wanajiona wana haki ya kupewa rushwa, mahakamani mafaili yanafichwa na hata polisi, sehemu ambazo zilipaswa kuwa mstari wa mbele kutetea haki ya mtu.
Kila mtu pale alipo aiangalie jamii yetu na matendo yake nyakati hizi, naweza kusema kuwa tunaishi katika jamii ya watu wanaopenda rushwa, maana hata bei za bidhaa zipande kiasi gani hakuna mtu anayethubutu kusema kwa sauti kuwa tunalanguliwa!
Kwa kweli inasikitisha  zaidi kwa namna Watanzania na serikali yao wanavyoonekana kwa taswira ya rushwa. Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika uhai wake na uongozi wake alikemea kwa vitendo rushwa na kwa kiasi kikubwa alifanikiwa kupunguza vitendo vya rushwa nchini.
 Kwa msimamo huo huduma za jamii kama vile elimu ilikidhi haja kwani wanafunzi walikuwa wakifundishwa na kugawiwa madaftari na hata kalamu bure, afya- watu walikuwa wakitibiwa bure na dawa zilikuwa zikipatikana, barabara- zilijengwa japokuwa kasi haikuwa kubwa, maji safi na salama yaliwafikia wananchi wengi vijijini bila mizengwe yoyote.
Sifa ya nchi ya Tanzania hakika ilikuwa nzuri machoni mwa wananchi na nje ya nchi. Ilikuwa ni vigumu kuona kiongozi wa serikali au shirika la umma akijenga hekalu ambalo halilingani na mshahara au kipato chake.
Leo hii kiongozi anaweza kusema kwenye bajeti ya serikali kuwa jengo fulani la serikali halitajengwa kwa kuwa bajeti haitoshi lakini huyohuyo akanunua magari yake mawili ya kifahari na kujenga nyumba mbili au tatu. Utajiuliza fedha amepata wapi? Jibu ni rahisi, ni rushwa tu.
Bahati mbaya baada ya uongozi wa Mwalimu, dhambi ya rushwa ikaanza taratibu kutambaa ndani ya jamii na sasa imekuwa kubwa mithili ya kansa isiyotibika. Tunashuhudia rushwa waziwazi katika chaguzi ambapo hata baadhi ya wana habari wanatajwa kujihusisha na rushwa. Hii ni mbaya sana. Wakati mwingine uhitaji hata ushahidi, maana maandishi yao na vitendo vyao vinajionesha.
Nimpongeze mwanahabari mkongwe, Jenerali Twaha  Ulimwengu ambaye amewataka wanahabari na wananchi wa Tanzania, hususan wale wanaokerwa na vitendo vya rushwa kukusanya hasira na kukemea kwa nguvu vitendo vya rushwa nchini, namuunga mkono mia kwa mia.
Alisema kuwa, kimsingi huwezi kupigana na mtu au nchi kama huna hasira, vivyohivyo inatupasa kuwa na hasira ya kutosha kupambana na adui huyu aitwaye rushwa ambaye kwa hakika amesababisha mabilioni ya shilingi za walipa kodi kupotea na kuingia katika mifuko ya watu binafsi wasio na huruma na wenzao.
Niseme bila kumung’unya maneno kwamba kama rushwa itaachiwa isambae bila kupigwa vita kwa nguvu, itamaliza taifa, tutateketea.
Jipu limepasuka, siwezi kuwa adui kwa kusema ukweli

Credits; www.globalpublisherstz.info

Sunday, July 22, 2012

HAKIMU ALIYETUHUMIWA KWA RUSHWA AACHIWA HURU HUKO MBEYA.

Habari na Ezekiel Kamanga,Mbeya.
Mahakama ya Hakimu Mfawidhi Wilaya ya Mbeya,umemwachia huru aliyekuwa Hakimu mkazi wa mahakama ya Mkoa wa Mbeya Amani Mwihomeke(30),aliyekuwa anakabiliwa na tuhuma za rushwa.

Hakimu huyo anakabiliwa na makosa mawili kinyume cha sheria kifungu cha 15 cha kanuni ya adhabu kifungu kidogo(i) cha 11/2007 ambapo alidaiwa kushawishi na kupokea rushwa ya shilingi 150,000 mnamo Mei 29 mwaka huu.

Mwendesha mashtaka wa Serikali kutoka kikosi cha kupambana na kuzuia rushwa nchini TAKUKURU,Kanda ya Mbeya Bwana Nimrod Mafwele akisaidiwa na Sarah Martin walidai Mahakamani kuwa Amani Mwihomeke alishawishi na kupokea rushwa hiyo katika Bar ya Bonanza iliyoko barabara ya Benki Kuu Jijini Mbeya.

Hakimu mfawidhi wa wilaya ya hiyo a Seif M. Kulita amesema mtuhumiwa anaachiwa huru kutokana na upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha tuhuma hizo hivyo mahakama kuchukua uamuzi huo wa hukumu ambayo ilichukua masaa matatu kusomwa katika mahakama hiyo.

Hakimu Mwihomeke alikuwa anatetewa wakili wa kujitegemea Mika Thadayo Mbise.

Hata hivyo Hakimu mfawidhi Kulita alitaka waeshesha mashtaka kuandaa vema mashtaka ambapo wameshindwa kuthibitisha tuhuma ambazo zingemtia mtuhumiwa hatiani.

Tuesday, July 3, 2012

MAKAMANDA WA JKT WAFIKISHWA MAHAKAMANI KWA UFISADI

ASKARI saba wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) wakiwamo Luteni Kanali watatu, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka ya kuhamisha na kupitisha Sh bilioni 3.8 kwa ajili ya ununuzi wa mali chakavu. Washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo jana asubuhi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), wakiwa kwenye gari aina ya Toyota Land Cruiser lenye namba za usajili T529 ASM lenye vioo vyeusi wakisindikizwa na gari lenye namba DFP 8763. Walisomewa mashitaka saba na mawakili kutoka Takukuru, Donasian Kessy na Ben Linkolin mbele ya Hakimu Mkazi Aloye Katema. Washitakiwa wenye cheo cha Luteni Kanali ni Mkohi Kichogo, Paul Mayavi na Felix Samillan ambaye ni Mkuu Miradi wa Suma JKT. Wengine ni Kanali Ayoub Mwakang’ata, Sajini John Laizer, Meja Peter Lushika na Meja Yohana Nyuchi. Wakili Kessy alidai kuwa, Machi 5, 2009 katika Ukumbi wa Mikutano wa Shirika la Suma JKT, washitakiwa wakiwa wajumbe wa Bodi ya Suma JKT, walijifanya wajumbe wa Bodi ya Kampuni ya Takopa inayoundwa kwa ubia kati ya Serikali ya Korea Kusini na Suma JKT. Alidai lengo la kujifanya wajumbe wa Bodi ya Takopa, lilikuwa kupitisha fedha kutoka kampuni hiyo kwenda Suma JKT kwa ajili ya ununuzi wa magari na mitambo ya ujenzi chakavu bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa kampuni hiyo. Wakili Kessy alidai kuwa washitakiwa walitumia vibaya ofisi kupitisha fedha hizo kwa ajili ya ununuzi wa magari pamoja na mitambo hiyo bila kufuata kifungu cha 58 (3) cha Sheria ya Manunuzi ya Umma. Aliendelea kudai katika mashitaka ya tatu yanayowakabili Luteni Kanali Samillan na Luteni Kanali Kichogo kuwa, Machi 16, 2009 walihamisha Sh bilioni 2.8 kupitia hundi namba 000010 kutoka akaunti ya Takopa namba 0111030331753 kwenda akaunti ya Suma JKT 01110307094 katika Benki ya Taifa ya Biashara (NBC). Ilidaiwa kuwa Aprili 3, 2009, wakijidai wajumbe wa Bodi hiyo ya Takopa walihamisha Sh milioni 489.7, Aprili 4 walihamisha Sh milioni 269.5, Mei 4, mwaka huo walihamisha Sh milioni 350 kutoka akaunti ya Takopa kwenda akaunti ya Suma JKT bila kuzingatia Kanuni ya 156 ya Sheria ya Fedha za Umma. Katika mashitaka ya saba yanayowakabili washitakiwa wote, ilidai kuwa kati ya Machi na Mei mwaka 2009 jijini Dar es Salaam, washitakiwa walipanga njama za kuhamisha fedha kutoka katika taasisi ya Takopa kwenda kwenye akaunti ya Suma JKT bila kufuata Kanuni 156 ya Sheria ya Fedha za Umma. Washitakiwa wote walikana kutenda makosa hayo na upande wa mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na kuwa hawana pingamizi la dhamana endapo washitakiwa watakidhi masharti yatakayotolewa na Mahakama. Hakimu Katemana aliwataka washitakiwa kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika watakaosaini hati ya Sh milioni 25 kila mmoja. Washitakiwa walitimiza masharti na kuachiwa kwa dhamana hadi Agosti mosi, mwaka huu. Hata hivyo, baada ya washitakiwa hao kufikishwa mahakamani hapo, hawakuwekwa mahabusu kama ilivyo kawaida kwa washitakiwa wengine, walikaa kwenye gari hadi saa 7 mchana waliposomewa mashitaka yao

Tuesday, June 19, 2012

DOLA MILIONI 148 HUVUSHWA NCHI ZA NG'AMBO KUTOKANA NA MIANYA YA RUSHWA TOKA AFRIKA.



ARUSHA
JUMLA ya  kiasi cha dola za Kimarekani Bilion 148   huwa zinapotea
ndani ya Nchi za bara la Afrika kila mwaka kutokana na kuwepo kwa
mianya mingi ya rushwa  na badala yake fedha hizo zinapelekwa katika
nchi za Ugaibuni hali ambayo inasababisha madhara makubwa sana kwa
nchi ya A frika


Hayo yameelezwa na mkurugenzi mkuu wa Taasisi ya kuzuia na kupambana
na Rushwa (TAKUKURU)Dkt Edward hosea wakati akizungumza katika mkutano
wa bodi ya ushauri wa masuala ya Rushwa kwa nchi za bara la Afrika
jijini hapa


Aidha dkt Hosea alisema kuwa kiwango hicho cha fedha hupotea kutokana
na baadhi ya mianya ya Rushwa ambayo imo kwenye nchi hizo na badala
yake fedha hizo zinapelekwa kwenye nchi za Ugaibuni


Alifafanua kuwa kutokana na hali hiyo ya upotevu wa fedha hizo
unachangia kwa kiwango kikubwa sana hata kukithiri kwa rushwa ndani ya
Nchi hizo hali ambayo nayo inachangia hata maendeleo duni ya nchi hizo
za bara la Afrika


“hiki ni kiwango kikubwa sana cha fedha ambazo zinapotea
kusikojulikana lakini mpaka sasa tumeshaanza kuweka mikakati
mbalimbali ya kuhakikisha kuwa nchi za bara la Afrika hazikumbwi na
rushwa ingawaje pia changamoto ya kupambana nayo ni kubwa
sana”Aliongeza Dkt Hosea.


Katika hatua nyingine alisema kuwa mpaka sasa kwa Upande wa Serikali
ya Tanzania tayari imeshatoa kiwanja kwa ajili ya   kujenga ofisi ya
bodi ya kupambana na Rushwa ambapo mchakato huo pia utasaidia sana
kupunguza wimbi kubwa sana la Rushwa hapa nchini.


Dkt Hosea alisisitiza kuwa ujenzi wa jengo hilo la  kupambana na
rushwa utaaanza mara baada ya bunge  Kupitisha bajeti yake ambapo
jengo hilo litajengwa ndani ya eneo la Kisongo mkoani Arusha


“kwa sasa tunafurai sana kwa kuwa ujenzi wa jengo hili umeshawekwa
katika mikakati na kitu ambacho tunasubiri ni bajeti yake na
tunachokiamini ni kuwa kupitia bodi hii tutaweza kuendelea kudhibiti
mianya ya rushwa ndani ya Nchi za bara la Afrika”aliongeza Dkt Hosea

Sunday, June 17, 2012

TAKUKURU NACHINGWEA YASHIRIKI KWENYE UELIMISHAJI UMMA WAKATI WA MBIO ZA MWENGE.

Viongozi wa ngazi ya wilaya wakishika Mwenge.


Umati ukishuhudia mwenge


Machapisho ya Takukuru yalioneshwa na kugawiwa kwa wananchi.


Uelimishaji umma ukiendelea na mtandao wa takukurunachi ulifunguliwa.

Wednesday, June 13, 2012

TAKUKURU LINDI YAFANYA MKUTANO NA MAHAKIMU WAKAZI WA WILAYA NA MKOANI LINDI.


Hakimu Mkuu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa wa Lindi Bw. Ndunguru(katikati) akiwa pamoja na Mratibu wa NACCSAP  wa Lindi Bw. Kuhanda (kushoto) na Bi. Lilian, Hakimu Mkazi Lindi wakisikiliza hoja mbalimbali za mkutano huo ulioitishwa na TAKUKURU Lindi ili kubadilishana uzoefu juu Uendeshaji kesi Mahakamani. Mkutano ulifanyika majuma mawili yaliyopita Ukumbi wa Takukuru Lindi


Wajumbe wa Mkutano huo wakimsikiliza Mh. Ndunguru akitoa mada yake juu ya Wajibu wa Mahakimu na Waendesha Mashtaka katika kutoa Haki.


Mafunzo yakiendelea.


Mahakimu Wakazi na Waendesha Mashtaka wakisikiliza.

Tuesday, June 12, 2012

UZINDUZI WA MBIO ZA MWENGE WA UHURU 2012 JIJINI MBEYA

 


Waziri Mkuu, Mizengo Pinda (katikati) akiwasha mwenge wa uhuru kuashiria kuanza kwa mbio za mwenge huo kwa mwaka 2012 leo katika uwanja wa kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya. Mwenge huo utakimbizwa kwenye jumla ya Halmashauri za wilaya, Manispaa na miji 157 na kuongozwa na kauli mbiu ya Sensa ya watu na Makazi ni Msingi wa Mipango ya Maendeleo yetu Shiriki kuhesabiwa Agosti 26.

Waziri Mkuu  Mizengo Pinda akikata utepe kuashiria uzinduzi wa vipeperushi vya elimu ya sensa ya watu na makazi itakayofanyika nchini kuanzia Agosti 26 mwaka huu wakati wa uzinduzi wa mbio za mwenge leo jijini Mbeya. Kushoto ni Kamishna wa Sensa kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Hajjat Amina Fatma Mrisho.

Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenela Mukangara (kushoto) akimtambulisha  kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda kiongozi wa mbio za mwenge mwaka 2012 Kepteni Honest Erenest Mwanossa kutoka Dar es salaam (kulia).
Kiongozi wa mbio za Mwenge Mwaka 2012, Kepteni Honest Erenest  Mwanossa kutoka Dar es salaam akikabidhi Mwenge wa Uhuru kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda tayari kwa kuukabidhi kwa viongozi wa Mkoa wa Mbeya tayari kwa kukimbizwa kwenye maeneo mbalimbali ya mkoa huo.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge Mwaka 2012, Kepteni Honest Erenest  Mwanossa (kulia) akikabidhi Mwenge wa Uhuru kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro tayari  kwa kukimbizwa kwenye maeneo mbalimbali ya mkoa huo kabla ya kuelekea mkoani Iringa

credits; mwaikenda