Thursday, November 6, 2014

WATALII WALALAMIKIA RUSHWA KATIKA VIZUIZI VYA BARABARANI HUKO ZANZIBAR.




KAMA vituo 66 vya treni havitoshi katika safari nzima ya utalii, Teresa Williamson wa  Australia na Annemarie Schuller wa Uholanzi wamesema Watanzania wanaishi katika mazingira magumu na wanastahili kubadilika.
 Kauli hiyo wameitoa wakati wakizungumza na Mwandishi wa makala haya muda mfupi kabla ya kuondoka kurejea makwao baada ya ziara ya wiki mbili katika maeneo mbalimbali nchini.
Katika ziara yao ya kitalii walitumia treni, barabara na maji tena kwa kutumia jahazi wakitokea Pangani Tanga hadi Zanzibar.
Nilitaka kujua baada ya utalii wao wameona nini nchini Tanzania walisema pamoja na kufanikiwa kuwaona wanyama wakubwa watano kama walivyofikiria wakati wakiwa makwao wameshuhudia maisha masikini zaidi kuliko matarajio.
“Sijui inatokeaje watu wengi wana simu za mkono lakini ukiangalia maisha yao unayaona kuwa magumu sana,” alisema Teresa ambaye alifafanua kwamba ugumu wa maisha unaonekana katika miundombinu na usafirishaji, ulaji na utunzaji wa mazingira.
Wakiwa wamezaliwa mjini hawakuwa wanajua vijijini kukoje mpaka walipofika nchini Tanzania na kukumbana na hali ambayo hawakuitarajia  hata kidogo.
Pamoja na kushuhudia matukio yasiyokuwa ya kawaida katika safari na mbugani ugumu wa maisha ambao wao wataendelea kuangalia ni mawasiliano, usafirishaji, na usalama.
Wamesema katika safari yao wamekumbana na tatizo  kubwa la chakula, usahihi wa taarifa na tatizo la mawasiliano.
“Pamoja na wananchi kuwa marafiki tumeona tatizo kubwa la usafiri na aina ya chakula kinacholiwa na usafi,” alisema Schuller ambaye kitaalamu ni mganga wa meno.
Kwa mtazamo wa watalii hao taifa hili linahitaji kubadili wananchi wake kwa kuwapa elimu ya kutosha kuhusu mazingira yanayowazunguka hasa kwa kujali aina ya mlo wanaokula, usafi wa mazingira na kujali gharama kwa huduma wanazotoa kwa wageni.
Teresa alisema kwa kuwa na aina moja ya chakula Ugali na wali muda wote bila maziwa mboga za majini kunatengeneza aina ya udumavu ambao unachochea watu kukosa lishe bora.
“Tumekuwa tukikumbana na chakula cha aina ile ile kila mahali tunapoenda, chakula cha nafaka ambacho ni wanga lakini hukutani na matunda, mboga za kijani na maziwa,” alisema Teresa.
Pamoja na kuzungumzia mlo, wageni hao walizungumzia  tatizo la rushwa na kusema walipokuwa Zanzibar pamoja na kuhisi kwamba ulinzi ni mkali kutokana na kusimamishwa kila mara katika gari, lakini waliona kuna kitu si sahihi wakati wa mazungumzo kati ya dereva na askari.
“Pale tuliona shida kidogo kwanini wanapenyeza mkono tena unaona kwa uangalifu mkubwa?” Alisema  Annemarie ambaye alisema matendo waliyokumbana nayo yanatia wasiwasi hasa unaposimamishwa mara saba katika kipindi cha dakika 40 wakati wakiwa kisiwa cha Zanzibar.
Kwao wanaamini kwamba lipo tatizo la rushwa na pia tatizo la lugha kwani wengi wameshindwa kuwasiliana nao kutokana na shida ya lugha kiasi ya kwamba wapo watu walikuwa wanawakwepa kwa sababu hawaelewani na wakati mwingine walifanya maamuzi ambayo hayakuwa sahihi kutokana na lugha gongana.
Anasema walipofika Tanga waliambiwa wanaweza kufika Zanzibar kupitia Pangani.Walisema usafiri uliwachosha na hata walipofika Pangani wakagundua kwamba mawasiliano si sahihi lakini wakaingia katika boti na kuelekea Zanzibar.
Boti hiyo ambayo ilikuwa kila mara inatolewa maji, iliwaogopesha sana lakini hata walipokuwa wakitaka kujua wanajiokoaje walijikuta wakiambulia kuambiwa kwamba njia za kujiokolea ni palepale walipo.
Hata hivyo walifarijika baada ya kugundua maboya ya kujiokolea ndio waliyoyakalia.
Pamoja na kufurahishwa na matembezi yao hasa kwa kuona kwamba wameweza kuwaona wanyama wakubwa kama tembo, chui, simba, faru,twiga na nyati walisema ipo haja ya kupunguzwa kwa kiingilio kwani kwa sasa wanakiona kama ghali.
Nilipomuuliza kuhusu Serengeti kama itakufa, alisema kwamba hadhani kwani anaona kwamba bado haijavurugwa sana na kama Watanzania watakubali kwamba ile ni mali yao haitakufa.
“Ni suala la kuelimika na kuhakikisha kwamba utamaduni unajali mazingira, unajali afya na wajibu,” alisema Teresa ambaye katika miaka yake 55 alisema Afrika bado ni bara la kutembelea.
Alisema walifika Sumve kuwaona jamaa zao na marafiki, lakini walishangazwa na wingi wa vituo ambapo treni inasimama japo waliona kwamba hali ile inaweza kuwa inasaidia mzunguko sahihi wa uchumi  wa eneo hilo.
“Njiani tuliona mengi lakini nadhani baya kabisa ni watu kutokujali mazingira yao. Uchafu unatupwa kila mahali na hata maeneo mengine hayakuwa na vyoo na yale yaliyokuwa na vyoo hata karatasi laini za chooni zilikosekana,” alisema Teresa.
Kwa maneno yao watu wanatakiwa kubadilika kupitia elimu ili kutambua kwamba kuna haja ya kuwa na mazingira safi kwa manufaa yao na kizazi kijacho.
“Unakosaje mahali pa kujisaidia? Umelipa fedha ili ufurahi inakuaje unapokosa huduma,” aliuliza Teresa.
Kwa maneno yao wenyewe ugumu wa kupata huduma inayoridhisha kwa fedha halisi  si tu katika maeneo waliyofikia bali hata katika usafiri.
“Ukiwa peke yako huwezi kufanikiwa,” alisema Teresa na kuungwa mkono na Annemarie ambaye yeye kuja Afrika ilikuwa mara yake ya kwanza. Moja ya tatizo ni kukosekana kwa uaminifu miongoni mwa watu wanaoandaa usafiri ambao wamekuwa wakiwatoza ada kubwa kuliko wanayokuja kujua baadaye.
Yalikuwa ni maoni ya mwandishi wa makala haya kwamba tatizo hilo linatokana na kutumia wakala katika masuala ya utalii na badala yake watu  ambao wamejitangaza kujua Tanzania na kwamba watawapokea.
Watu hao ambao unaweza kulinganisha na vishoka wanachojali wao ni kuongeza cha juu na kuwafikisha watalii wao katika maeneo ambayo ni rahisi na wakati mwingine bila kuwa na muunganisho mwema.
Pamoja na udhaifu katika masuala ya utalii hasa mawasiliano na upashanaji wa taarifa elimu inayotakiwa miongoni mwa wananchi ni kubadili masuala yao yanayowafanya wawe na maisha magumu.
Kwa watalii hao wamesema hawajawahi kuona ardhi yenye rutuba kubwa kama Tanzania na kinachotakiwa kufanywa ni watu wake kutumia fursa zilizopo kujikwamua katika dhiki ya umasikini na kuboresha maisha yao.
Walielezea kufurahishwa na ukarimu uliofanywa na Wapare walipoenda kutembelea eneo la Mbagha ambako walilala Tona Lodge na kupata maelezo kuhusu kijiji na kutembelea vivutio mbalimbali likiwemo jiwe lililotumika kuua watoto waliokuwa wanafikiriwa wana mikosi.
Naam, mpaka mwisho wa mazungumzo wageni hao walilalamikia usafi, utunzaji wa mazingira, mfumo wa lishe na mawasiliano hafifu pamoja na lugha gongana unaleta utata wa uaminifu.

Sunday, June 16, 2013

DK. HOSSEAH WA TAKUKURU AFUNGUKA, ASEMA TAKUKURU INATENGWA NA SERIKALI.



Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah 

Dodoma. Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah, amefunguka na kueleza sababu za taasisi yake kushindwa kuwakamata walarushwa wakubwa kwa kuwa Serikali imemfunga mikono.
Akitoa majumuisho katika Mkutano Mkuu wa Chama cha Wabunge Wanaopambana na Rushwa nchini (APNAC) jana, Dk Hoseah alisema kuwa Serikali imeitenga Takukuru na kuwafanya waishi kama yatima.
Huku akishangiliwa na idadi kubwa ya wabunge, mkurugenzi huyo alisema kuwa amekuwa akishangazwa na lawama ambazo amekuwa akibebeshwa kila wakati kuwa ameshindwa kumaliza rushwa wakati bila kuziangalia sheria.
“Mnanipa lawama kila wakati, lakini huwezi kuanzisha chombo kama Takukuru halafu ukamfunga mikono mhusika, na mimi mmenifunga mikono nifanyeje jamani? Alihoji na kuongeza:
“Hata katika rasimu ya Katiba bado mmetutenga kama watoto yatima, wenzetu wote mmewaweka tena hata CAG mmesema kuwa mamlaka yake akiteuliwa basi asiingiliwe wala kuhojiwa…mamlaka gani mtu asihojiwe jamani, mimi nikiuliza Takukuru mnasema subirini Serikali ya Tanganyika.”
Gazeti la Guardian la Uingereza la Jumapili ya Desemba 19, 2010, lilitoa taarifa ya siri kuhusu wala rushwa wakubwa kulindwa Tanzania. Gazeti hilo lilichapisha taarifa za mtandao wa WikiLeaks uliokuwa ukimilikiwa na mwandishi wa habari wa Australia, Julian Paul Assange, ukimnukuu Dk Hoseah.
Dk Hoseah alinukuliwa na WikiLeaks akimueleza mwanadiplomasia wa Marekani aitwaye Purnell Delly, Julai 14 jijini Dar es Salaam mwaka 2007 kuhusu uwezo na nia ya Rais Kikwete katika kushughulikia ufisadi.
Alidai Rais Jakaya Kikwete alikuwa anakwamisha kuchunguzwa kwa vigogo wa Serikali wanaotuhumiwa kwa vitendo vya rushwa, na pia anahofia maisha yake kama mkuu wa Takukuru. Hata hivyo, Dk Hoseah kwanza alikiri kukutana na ofisa huyo ofisini kwake Julai 2007, lakini alikanusha kuzungumza kuwa Rais Kikwete alikuwa hataki sheria ichukue mkondo wake katika kuwachunguza vigogo wanaotuhumiwa kwa rushwa.
Atoa ushauri kwa Serikali
Kwa mara ya kwanza jana kiongozi huyo aliitolea uvivu Serikali kuwa imekuwa ikichangia mambo mengi katika rushwa ikiwamo usiri mkubwa katika rasilimali za nchi.
“Lazima Serikali iwe wazi, huwezi kuwaficha wananchi rasilimali zao eti ni siri kwa sababu ya sera mbovu, tunawaambia wananchi watanufaika na mirabaha ya asilimia tatu hiyo siyo sahihi jamani ndiyo maana tunashindwa kutoa majibu kwa wananchi wetu hilo ni tatizo jingine linalosababisha mambo ya rushwa,”alisema na kuongeza: “Siyo kila jambo ambalo serikali inapewa ushauri ni baya.”
Alipinga kitendo cha viongozi kuwa na kigugumizi katika uwajibikaji na akataka itungwe sheria kali ya kutaka kiongozi awajibike mara anapokuwa ametuhumiwa kwa jambo lolote aachie ngazi na kupisha uchunguzi kama ilivyo kwa nchi zingine.
Credits; Gazeti la Mwananchi

ELIMU YA NAMNA YA KUEPUKA RUSHWA KWA SEKTA YA AFYA WILAYANI NACHINGWEA.

 Wadau wa Afya toka maeneo mbalimbali ya Nachingwea walikutana katika Ukumbi wa TRC mjini Nachingwea na moja ya somo walilofundishwa ni Mapambano dhidi ya Rushwa.

Wanafunzi Chuo cha UUguzi Nachingwea wakipata elimu ya Mapambano dhidi ya Rushwa toka kwa Maafisa wa TAKUKURU waliowatembelea hivi karibuni.

ELIMU YA MAPAMBANO DHIDI YA RUSHWA YATOLEWA KWA WANAFUNZI WA SEKONDARI WILAYANI NACHINGWEA.

 

Afisa wa TAKUKURU Bw. Hassan Omari wa Nachingwea akipokea risala toka kwa kiongozi wa Klabu ya Wapinga wa Rushwa shule ya sekondari Marambo wakati wa ziara ya uhamasishaji wa mapambano dhidi ya rushwa hivi karibuni.

Baadhi ya wanafunzi shule ya sekondari Marambo huko Nachingwea wakisikiliza mawaidha toka kwa maafisa wa TAKUKURU(hawapo pichani).

Wednesday, November 14, 2012

MBOWE KUIFUTA TAKUKURU MARA AKIINGIA MADARAKANI.

MBOWE ASEMA CHADEMA IKICHUKUA MADARAKA ITATIMUA WATENDAJI WOTE WA TAKUKURU KWA VILE WAMESHINDWA KUZUIA RUSHWA CCM.


Mwenyekiti wa chadema,Freeman Mbowe akiwa na keki aliyokabidhiwa na wakulima wa ngano Babati,ambao walimuomba awasaidie kutetea kurejeshwa mashamba ya Ngano yaliyokuwa na shirika la chakula la Taifa(NAFCO) ambayo sasa yamebinafsishwa na hayaendelezwi. Kulia ni   diwani wa viti maalum Hanang, Sara Joseph

Mwandishi wetu, Hanang’
MWENYEKITI wa Chadema, Freeman Mbowe amependekeza kuvunjwa kwa Taasisi za Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kwani badala ya kupambana nayo inaipalilia.
Akifungua tawi ya Chadema Kata za Katesh linalopakana na ofisi za Takukuru Wilaya ya Hanang, Mkoa wa Manyara juzi, Mbowe alisema taasisi hiyo imeshindwa kazi.


Mbowe alisema Takukuru imeshindwa kudhibiti hata rushwa ya wazi ndani ya CCM kwenye chaguzi ambazo zilifanyika hivi karibuni.
“Hakuna ambaye hakujua rushwa ndani na CCM na jinsi ambavyo imeathiri chama hicho, lakini Takukuru wameshindwa kupambana na rushwa hiyo badala yake wanailea,” alisema Mbowe.


Alisema Rais Jakaya Kikwete ambaye anasimamia Takukuru iliyopo kwenye wizara yake, ameshindwa kuibana ndiyo sababu hata yeye amekuwa akilalamika.
Pia, Mbowe alifungua matawi kata za Endasaki na Ganana, alisema kutokana na Takukuru kushindwa kupambana na rushwa, isipovunjwa chama hicho kikiingia madarakani kitawatimua watendaji wote wa taasisi hiyo ili wafanye kazi nyingine.


Alisema Takukuru imeshindwa hata kusaidia kurejesha mabilioni ya fedha za Watanzania ambayo yamefichwa nchini Uswis.


“Hawa Takukuru walipaswa kuanza kufanya uchunguzi juu ya fedha hizo baada ya kupata taarifa na kusaidia taifa kuzipata, lakini wamekaa kimya,” alisema Mbowe.


Alisema kutokana na ukimya huo, ndiyo sababu Chadema kupitia Naibu Katibu Mkuu wake, Kabwe Zitto waliomba serikali kufanya uchunguzi na kutoa taarifa bungeni juu ya walioficha fedha na utaratibu wa kuzirejesha.


“Bunge lijalo, kama wasipoleta taarifa ya maana juu ya fedha za Uswis tunajua la kufanya, nadhani mmeona jinsi hoja hii ilivyoungwa mkono na watu wengi,”alisema Mbowe.


Awali, Mbowe alizitaka ofisi hizo za Chadema, alizofungua kuwa kimbilio la wanyonge kutoa kero zao na kusaidiwa badala ya kuwa maeneo ya kukaa viongozi pekee.
Chanzo. Gazeti la Mwananchi

Sunday, November 4, 2012

MBUNGE ZUNGU WA ILALA AKAMATWA KWA RUSHWA

 

Mbunge Zungu wa Ilala Anaswa Akitoa Rushwa

NewsImages/6661242.jpg
Mbunge wa Ilala, Musa Zungu
Watu watano akiwemo mbunge wa Ilala Musa Zungu wamekamatwa na Taasisi ya kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoani Dodoma wakidaiwa kutoa rushwa kwa wajumbe wa Jumuiya ya wazazi ili wawachague.
Kamanda wa Taasisi hiyo Eunice Mmari alisema Zungu alikamatwa katika Hotel ya Golden Crown majuzi kati ya saa mbili na nusu na saa tatu usiku.

Eunice alisema baa ya taasisi yake kupata taarifa hizo walianza kumfuatilia kwa karibu mgombea huyo na ndipo walipomsikia akitoa maagizo kupitia simu ya mkononi kuagizia nani apewe kiasi gani.

Alisema baada ya hatua hiyo TAKUKURU walianza kumfatilia Zungu na ndipo waligundua kuwa yupo katika gari ndogo aina ya Toyota Mark –II huku akifuatana na gari jingine aina ya Prado ambalo ndiko fedha na wapambe wake walikuwa wamepanda.

Alisema baada ya kulisimamisha gari hilo alilokuwemo Zungu ghafla Prado hilo liliweza kutoroka na kumuacha Zungu na ndipo alipokamtwa na kuhojiwa.

Alisema hata hivyo TAKUKURU waliweza kufuatilia mitandao ya simu na kisha kubaini kuwa fedha hizo zilikuwa zikigawiwa na mmoja wa wakala wake ambaye naye kwa sasa amekamtwa.

Kamanda huyo aliwataja wengine waliokamatwa na Zungu ni pamoja na Yahya Khamis Danga , Busulo Mohamed Pazi na Famik Joseph Mang’ati.

Alisema kwa sasa watuhumiwa hao wote wameachiwa kwa dhamana huku uchunguzi zaidi ukiendelea na watafikishwa mahakamani mara baada ya kukamilika.

Aidha kamanda huyo alisema mwingine aliyekamtwa ni pamoja na Fatuma Kasenga ambaye ni mwenyekiti wa jumuiya ya Wazazi kutoka Mkoa wa Mbeya.

Alisema mwenyekiti huyo alikamatwa usiku wa kuamkia juzi, saa tisa usiku katika hoteli ya Kitoli mjini hapa akiwanunulia wajumbe wake chakula.

Kamanda huyo apia alisema kuna taarifa zaidi ambazo zinamtaja Alhaji Abdalah Bulembo kuwa naye amekuwa akitajwa sana katika utoaji huo wa rushwa.

Alisema hata hivyo wanaendelea na uchunguzi dhidi ya tuhuma za Bulembo na wamepata taarifa za awali kuwa anatoa rushwa hizo nyumbani.

Tuesday, September 25, 2012

HAKIMU WA ILALA ASOMEWA MASHTAKA YA RUSHWA KISUTU.

Hakimu na Rushwa                                                                    

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala Pamela Kalala (kushoto),akitoka katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam jana,baada ya kusomewa shitaka la kuomba rushwa ya Shilingi milioni tatu.Picha na Michael Matemanga

Sunday, September 9, 2012

WAZIRI MKUU MSTAAFU AMEITAKA AFRIKA IPAMBANE NA RUSHWA, AMERIDHISHWA NA UTENDAJI KAZI WA TAKUKURU.

Sumaye ameitaka Afrika kutokomeza rushwa

 
Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye amezitaka nchi za Afrika ikiwemo Tanzania kupambana na makundi na kuwalipua wala rushwa na wapokeaji kwa kuwachukulia hatua.
Alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam katika maadhimisho ya miaka 20 ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, (OUT).
Katika mada yake iliyokuwa ikizungumzia kuhusu changamoto za kupunguza umaskini nchini, Sumaye alisema nchi za Afrika zipo nyuma kimaendeleo na kwamba yapo mambo mengi yanayotakiwa kufanyika.
Alitaja baadhi ya mambo hayo kuwa ni nchi kuwa na serikali inayopambana na makundi yote mabaya hasa rushwa.
"Lazima tuipige vita rushwa ili kile kidogo kinachotakiwa kipatikane basi kipatikane kwa ajili ya huduma za wananchi na sio kupotea njia," alisema.
Alitaka nchi zifanye biashara ambazo zitaweza kuzimudu na kutolea mfano Tanzania.
"Tusiuze tu vitu kwa mfano magogo, pamba na madini nje ya nchi, tunatakiwa vitu hivi tuvibadilishe kuwa thamani ndio tuvipeleke nje kwenye soko la biashara, tunaiuzia magogo China halafu yeye anayabadilisha kuwa vitu vya thamani anakuja kutuuzia sisi tena, kwa nini sisi tusifanye vyote hivyo, tuwauzie wao," alisema.
Kuhusu rushwa na utawala bora, Sumaye alisema lazima nchi ifikie mahali iwe na utaratibu wa kuhakikisha jambo hilo halivumiliki kwa sababu limekuwa likiigawa jamii katika kundi la wenye utajiri na maskini.
Mtazamo wake kama Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa sasa inafanya kazi yake ipasavyo kutokana na kuanzishwa wakati akiwa madarakani, alisema anafikiri inafanya kazi yake.
Kuhusu nini kifanyike, Sumaye alisema nchi inatakiwa kuwa na utawala bora ambao utawezesha rasilimali za nchi zinatumika kwa manufaa ya watu wote.
Pia alisema nchi inatakiwa kuhakikisha inakuwa na utawala wa sheria na kuheshimu haki za binadamu na kuwepo na matumizi sahihi ya mali za taifa ili kila Mtanzania aweze kunufaika nazo.
Naye, Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Tolly Mbwette, alisema kuwa, katika maadhimisho hayo miadhara ya majadiliano iliyotolewa imelenga jamii na serikali kwa ujumla.
Alisema lengo lake ni kutoa michango yao kwenye maeneo tofauti ambayo serikali imejiwekea katika kuyafikia maendeleo.
Profesa Joseph Mbwiriza wa OUT akichangia majadiliano hayo, alisema suala la umaskini ni kubwa na watu wengi wapo nje ya mfumo rasmi wa uchumi.
"Wanawake wengi hatuwatambui, kazi wanazozifanya haziingii kwenye takwimu zetu za kiuchumi za taifa, nini kifanyike tutekeleze Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (Mkurabita) ili kazi zao na za wengine zitambuliwe kisheria, " alisema.
Katika maadhimisho hayo mijadala mbalimbali ilitolewa ukiwemo uliokuwa ukiangalia kupotea kwa maadili kwenye jamii ya Tanzania.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

Thursday, September 6, 2012

JUSTUS KATITI THE FORMER TRA ACCOUNTANT ACQUITED IN SOME CHARGES OF FORGERY AND MONEY LAUNDERING

 

MHASIBU TRA AACHIWA HURU NA MAHAKAMA YA KISUTU, LAKINI YUPO RUMANDE AKIKABILIWA NA MASHTAKA MENGINE.
Dar es Salaam.  The former Tanzania Revenue Authority (TRA) accountant, Mr Justus Katiti, and four others were yesterday acquitted by the Kisutu Resident Magistrate’s Court of 10 charges including money laundering.
Mr Katiti and his co-accused were set free after a judgment read by magistrate Aloyce Katemana for more than an hour concluding that the prosecution had failed to prove the charges against the accused beyond reasonable doubt.
“There is no weighty evidence produced to the court that proves the charges against the accused. So, the court sees that the accused are not guilty of the offences and thus the court dismisses all the charges and sets them free,” the magistrate ruled.
However, the accused will remain in the remand prison because they are facing other money laundering charges at the same court.
Mr Katiti and his co-accused were facing 10 counts including conspiracy, forgery and falsely obtaining the money between September and October 2008, the property of Barclays Bank Tanzania.
Other accused in the case are Fortunatus Muganzi and Godwin Paula, who were employees of the bank and businessmen Gidon Utulo and Robert Mbetwa.
During the hearing of the case, the prosecution produced 28 witnesses along with several evidence to support their case. The accused were charged that between September 29, and October 6, 2008, they stole from the bank.
The accused allegedly forged a Barclays Bank form number E.7 to show that Tourism Promotion Services (Tanzania) Limited requested the bank to pay Sh338,935,337.46 to East Africa Procurement Services Limited for selling them hotel equipment.
They were also charged to have uttered the forged form to the Barclays head office in Ilala and obtained the money.
Another count facing Mr Katiti is that, being a TRA employee with intend to defraud prepared and uttered false information to show that the Tourism Promotion Company paid the sum amount as VAT while he knew to be false.
The accused also allegedly transferred the money from the Tourism Promotion Company account at CRDB Bank to Barclays Bank and distributed it to various individual accounts before they withdrew the money

Tuesday, August 21, 2012

MKOMBOZI WA TANZANIA TOKA MAKUCHA YA RUSHWA NI MTANZANIA MWENYEWE.

 Nani ataikomboa Tanzania kwenye makucha ya rushwa?

Jenerali Ulimwengu.
HATA kwenye maandiko ya vitabu vitakatifu tunaambiwa kuwa, Mwenyezi Mungu baada ya uumbaji wa dunia alimweka Adamu na Hawa katika Bustani ya Edeni na kuwapa uhuru wa kula matunda yote katika  bustani ile isipokuwa matunda ya mti uliokuwepo katikati ya bustani.
Kwa wanaofuatilia maandiko ya dini wanafahamu kilichotokea. Hapa nchini kuna sheria na maneno mengi yanayowataka viongozi na raia wa kawaida kutojihusisha na vitendo vya rushwa.
Lakini ajabu ni kwamba hivi majuzi tumesikia shutuma nzito za vitendo vya rushwa zikitolewa ndani ya Bunge vikiwahusisha viongozi wa Kamati za Bunge hususan Kamati ya Nishati na Madini, Hesabu za Serikali za Mitaa na Hesabu ya Mashirika ya Umma.
Kiukweli  tunachokiona si cha ajabu, maana ni taswira ya mambo ambayo sisi kama jamii tumeyakubali, tumeyapokea na kuyafanya kuwa sehemu ya maisha yetu. Limekuwa ni jambo la kawaida mtumishi fulani kula rushwa na kujitajirisha harakaharaka na watu kumsifu kwamba eti ana akili sana!
Katika baadhi ya vitengo kama vile mahakamani, polisi, idara za ardhi au maliasili kama ambavyo iliwahi kuaninishwa na Tume ya Joseph Warioba, ulaji wa mlungula ni  tabia ambayo baada ya muda imegeuka na kuwa ‘mazoea’ na hatimaye kuwa haki.
Wanaofanya hivyo wanajiona wana haki ya kupewa rushwa, mahakamani mafaili yanafichwa na hata polisi, sehemu ambazo zilipaswa kuwa mstari wa mbele kutetea haki ya mtu.
Kila mtu pale alipo aiangalie jamii yetu na matendo yake nyakati hizi, naweza kusema kuwa tunaishi katika jamii ya watu wanaopenda rushwa, maana hata bei za bidhaa zipande kiasi gani hakuna mtu anayethubutu kusema kwa sauti kuwa tunalanguliwa!
Kwa kweli inasikitisha  zaidi kwa namna Watanzania na serikali yao wanavyoonekana kwa taswira ya rushwa. Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika uhai wake na uongozi wake alikemea kwa vitendo rushwa na kwa kiasi kikubwa alifanikiwa kupunguza vitendo vya rushwa nchini.
 Kwa msimamo huo huduma za jamii kama vile elimu ilikidhi haja kwani wanafunzi walikuwa wakifundishwa na kugawiwa madaftari na hata kalamu bure, afya- watu walikuwa wakitibiwa bure na dawa zilikuwa zikipatikana, barabara- zilijengwa japokuwa kasi haikuwa kubwa, maji safi na salama yaliwafikia wananchi wengi vijijini bila mizengwe yoyote.
Sifa ya nchi ya Tanzania hakika ilikuwa nzuri machoni mwa wananchi na nje ya nchi. Ilikuwa ni vigumu kuona kiongozi wa serikali au shirika la umma akijenga hekalu ambalo halilingani na mshahara au kipato chake.
Leo hii kiongozi anaweza kusema kwenye bajeti ya serikali kuwa jengo fulani la serikali halitajengwa kwa kuwa bajeti haitoshi lakini huyohuyo akanunua magari yake mawili ya kifahari na kujenga nyumba mbili au tatu. Utajiuliza fedha amepata wapi? Jibu ni rahisi, ni rushwa tu.
Bahati mbaya baada ya uongozi wa Mwalimu, dhambi ya rushwa ikaanza taratibu kutambaa ndani ya jamii na sasa imekuwa kubwa mithili ya kansa isiyotibika. Tunashuhudia rushwa waziwazi katika chaguzi ambapo hata baadhi ya wana habari wanatajwa kujihusisha na rushwa. Hii ni mbaya sana. Wakati mwingine uhitaji hata ushahidi, maana maandishi yao na vitendo vyao vinajionesha.
Nimpongeze mwanahabari mkongwe, Jenerali Twaha  Ulimwengu ambaye amewataka wanahabari na wananchi wa Tanzania, hususan wale wanaokerwa na vitendo vya rushwa kukusanya hasira na kukemea kwa nguvu vitendo vya rushwa nchini, namuunga mkono mia kwa mia.
Alisema kuwa, kimsingi huwezi kupigana na mtu au nchi kama huna hasira, vivyohivyo inatupasa kuwa na hasira ya kutosha kupambana na adui huyu aitwaye rushwa ambaye kwa hakika amesababisha mabilioni ya shilingi za walipa kodi kupotea na kuingia katika mifuko ya watu binafsi wasio na huruma na wenzao.
Niseme bila kumung’unya maneno kwamba kama rushwa itaachiwa isambae bila kupigwa vita kwa nguvu, itamaliza taifa, tutateketea.
Jipu limepasuka, siwezi kuwa adui kwa kusema ukweli

Credits; www.globalpublisherstz.info

Sunday, July 22, 2012

HAKIMU ALIYETUHUMIWA KWA RUSHWA AACHIWA HURU HUKO MBEYA.

Habari na Ezekiel Kamanga,Mbeya.
Mahakama ya Hakimu Mfawidhi Wilaya ya Mbeya,umemwachia huru aliyekuwa Hakimu mkazi wa mahakama ya Mkoa wa Mbeya Amani Mwihomeke(30),aliyekuwa anakabiliwa na tuhuma za rushwa.

Hakimu huyo anakabiliwa na makosa mawili kinyume cha sheria kifungu cha 15 cha kanuni ya adhabu kifungu kidogo(i) cha 11/2007 ambapo alidaiwa kushawishi na kupokea rushwa ya shilingi 150,000 mnamo Mei 29 mwaka huu.

Mwendesha mashtaka wa Serikali kutoka kikosi cha kupambana na kuzuia rushwa nchini TAKUKURU,Kanda ya Mbeya Bwana Nimrod Mafwele akisaidiwa na Sarah Martin walidai Mahakamani kuwa Amani Mwihomeke alishawishi na kupokea rushwa hiyo katika Bar ya Bonanza iliyoko barabara ya Benki Kuu Jijini Mbeya.

Hakimu mfawidhi wa wilaya ya hiyo a Seif M. Kulita amesema mtuhumiwa anaachiwa huru kutokana na upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha tuhuma hizo hivyo mahakama kuchukua uamuzi huo wa hukumu ambayo ilichukua masaa matatu kusomwa katika mahakama hiyo.

Hakimu Mwihomeke alikuwa anatetewa wakili wa kujitegemea Mika Thadayo Mbise.

Hata hivyo Hakimu mfawidhi Kulita alitaka waeshesha mashtaka kuandaa vema mashtaka ambapo wameshindwa kuthibitisha tuhuma ambazo zingemtia mtuhumiwa hatiani.

Tuesday, July 3, 2012

MAKAMANDA WA JKT WAFIKISHWA MAHAKAMANI KWA UFISADI

ASKARI saba wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) wakiwamo Luteni Kanali watatu, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka ya kuhamisha na kupitisha Sh bilioni 3.8 kwa ajili ya ununuzi wa mali chakavu. Washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo jana asubuhi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), wakiwa kwenye gari aina ya Toyota Land Cruiser lenye namba za usajili T529 ASM lenye vioo vyeusi wakisindikizwa na gari lenye namba DFP 8763. Walisomewa mashitaka saba na mawakili kutoka Takukuru, Donasian Kessy na Ben Linkolin mbele ya Hakimu Mkazi Aloye Katema. Washitakiwa wenye cheo cha Luteni Kanali ni Mkohi Kichogo, Paul Mayavi na Felix Samillan ambaye ni Mkuu Miradi wa Suma JKT. Wengine ni Kanali Ayoub Mwakang’ata, Sajini John Laizer, Meja Peter Lushika na Meja Yohana Nyuchi. Wakili Kessy alidai kuwa, Machi 5, 2009 katika Ukumbi wa Mikutano wa Shirika la Suma JKT, washitakiwa wakiwa wajumbe wa Bodi ya Suma JKT, walijifanya wajumbe wa Bodi ya Kampuni ya Takopa inayoundwa kwa ubia kati ya Serikali ya Korea Kusini na Suma JKT. Alidai lengo la kujifanya wajumbe wa Bodi ya Takopa, lilikuwa kupitisha fedha kutoka kampuni hiyo kwenda Suma JKT kwa ajili ya ununuzi wa magari na mitambo ya ujenzi chakavu bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa kampuni hiyo. Wakili Kessy alidai kuwa washitakiwa walitumia vibaya ofisi kupitisha fedha hizo kwa ajili ya ununuzi wa magari pamoja na mitambo hiyo bila kufuata kifungu cha 58 (3) cha Sheria ya Manunuzi ya Umma. Aliendelea kudai katika mashitaka ya tatu yanayowakabili Luteni Kanali Samillan na Luteni Kanali Kichogo kuwa, Machi 16, 2009 walihamisha Sh bilioni 2.8 kupitia hundi namba 000010 kutoka akaunti ya Takopa namba 0111030331753 kwenda akaunti ya Suma JKT 01110307094 katika Benki ya Taifa ya Biashara (NBC). Ilidaiwa kuwa Aprili 3, 2009, wakijidai wajumbe wa Bodi hiyo ya Takopa walihamisha Sh milioni 489.7, Aprili 4 walihamisha Sh milioni 269.5, Mei 4, mwaka huo walihamisha Sh milioni 350 kutoka akaunti ya Takopa kwenda akaunti ya Suma JKT bila kuzingatia Kanuni ya 156 ya Sheria ya Fedha za Umma. Katika mashitaka ya saba yanayowakabili washitakiwa wote, ilidai kuwa kati ya Machi na Mei mwaka 2009 jijini Dar es Salaam, washitakiwa walipanga njama za kuhamisha fedha kutoka katika taasisi ya Takopa kwenda kwenye akaunti ya Suma JKT bila kufuata Kanuni 156 ya Sheria ya Fedha za Umma. Washitakiwa wote walikana kutenda makosa hayo na upande wa mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na kuwa hawana pingamizi la dhamana endapo washitakiwa watakidhi masharti yatakayotolewa na Mahakama. Hakimu Katemana aliwataka washitakiwa kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika watakaosaini hati ya Sh milioni 25 kila mmoja. Washitakiwa walitimiza masharti na kuachiwa kwa dhamana hadi Agosti mosi, mwaka huu. Hata hivyo, baada ya washitakiwa hao kufikishwa mahakamani hapo, hawakuwekwa mahabusu kama ilivyo kawaida kwa washitakiwa wengine, walikaa kwenye gari hadi saa 7 mchana waliposomewa mashitaka yao

Tuesday, June 19, 2012

DOLA MILIONI 148 HUVUSHWA NCHI ZA NG'AMBO KUTOKANA NA MIANYA YA RUSHWA TOKA AFRIKA.



ARUSHA
JUMLA ya  kiasi cha dola za Kimarekani Bilion 148   huwa zinapotea
ndani ya Nchi za bara la Afrika kila mwaka kutokana na kuwepo kwa
mianya mingi ya rushwa  na badala yake fedha hizo zinapelekwa katika
nchi za Ugaibuni hali ambayo inasababisha madhara makubwa sana kwa
nchi ya A frika


Hayo yameelezwa na mkurugenzi mkuu wa Taasisi ya kuzuia na kupambana
na Rushwa (TAKUKURU)Dkt Edward hosea wakati akizungumza katika mkutano
wa bodi ya ushauri wa masuala ya Rushwa kwa nchi za bara la Afrika
jijini hapa


Aidha dkt Hosea alisema kuwa kiwango hicho cha fedha hupotea kutokana
na baadhi ya mianya ya Rushwa ambayo imo kwenye nchi hizo na badala
yake fedha hizo zinapelekwa kwenye nchi za Ugaibuni


Alifafanua kuwa kutokana na hali hiyo ya upotevu wa fedha hizo
unachangia kwa kiwango kikubwa sana hata kukithiri kwa rushwa ndani ya
Nchi hizo hali ambayo nayo inachangia hata maendeleo duni ya nchi hizo
za bara la Afrika


“hiki ni kiwango kikubwa sana cha fedha ambazo zinapotea
kusikojulikana lakini mpaka sasa tumeshaanza kuweka mikakati
mbalimbali ya kuhakikisha kuwa nchi za bara la Afrika hazikumbwi na
rushwa ingawaje pia changamoto ya kupambana nayo ni kubwa
sana”Aliongeza Dkt Hosea.


Katika hatua nyingine alisema kuwa mpaka sasa kwa Upande wa Serikali
ya Tanzania tayari imeshatoa kiwanja kwa ajili ya   kujenga ofisi ya
bodi ya kupambana na Rushwa ambapo mchakato huo pia utasaidia sana
kupunguza wimbi kubwa sana la Rushwa hapa nchini.


Dkt Hosea alisisitiza kuwa ujenzi wa jengo hilo la  kupambana na
rushwa utaaanza mara baada ya bunge  Kupitisha bajeti yake ambapo
jengo hilo litajengwa ndani ya eneo la Kisongo mkoani Arusha


“kwa sasa tunafurai sana kwa kuwa ujenzi wa jengo hili umeshawekwa
katika mikakati na kitu ambacho tunasubiri ni bajeti yake na
tunachokiamini ni kuwa kupitia bodi hii tutaweza kuendelea kudhibiti
mianya ya rushwa ndani ya Nchi za bara la Afrika”aliongeza Dkt Hosea

Sunday, June 17, 2012

TAKUKURU NACHINGWEA YASHIRIKI KWENYE UELIMISHAJI UMMA WAKATI WA MBIO ZA MWENGE.

Viongozi wa ngazi ya wilaya wakishika Mwenge.


Umati ukishuhudia mwenge


Machapisho ya Takukuru yalioneshwa na kugawiwa kwa wananchi.


Uelimishaji umma ukiendelea na mtandao wa takukurunachi ulifunguliwa.

Wednesday, June 13, 2012

TAKUKURU LINDI YAFANYA MKUTANO NA MAHAKIMU WAKAZI WA WILAYA NA MKOANI LINDI.


Hakimu Mkuu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa wa Lindi Bw. Ndunguru(katikati) akiwa pamoja na Mratibu wa NACCSAP  wa Lindi Bw. Kuhanda (kushoto) na Bi. Lilian, Hakimu Mkazi Lindi wakisikiliza hoja mbalimbali za mkutano huo ulioitishwa na TAKUKURU Lindi ili kubadilishana uzoefu juu Uendeshaji kesi Mahakamani. Mkutano ulifanyika majuma mawili yaliyopita Ukumbi wa Takukuru Lindi


Wajumbe wa Mkutano huo wakimsikiliza Mh. Ndunguru akitoa mada yake juu ya Wajibu wa Mahakimu na Waendesha Mashtaka katika kutoa Haki.


Mafunzo yakiendelea.


Mahakimu Wakazi na Waendesha Mashtaka wakisikiliza.

Tuesday, June 12, 2012

UZINDUZI WA MBIO ZA MWENGE WA UHURU 2012 JIJINI MBEYA

 


Waziri Mkuu, Mizengo Pinda (katikati) akiwasha mwenge wa uhuru kuashiria kuanza kwa mbio za mwenge huo kwa mwaka 2012 leo katika uwanja wa kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya. Mwenge huo utakimbizwa kwenye jumla ya Halmashauri za wilaya, Manispaa na miji 157 na kuongozwa na kauli mbiu ya Sensa ya watu na Makazi ni Msingi wa Mipango ya Maendeleo yetu Shiriki kuhesabiwa Agosti 26.

Waziri Mkuu  Mizengo Pinda akikata utepe kuashiria uzinduzi wa vipeperushi vya elimu ya sensa ya watu na makazi itakayofanyika nchini kuanzia Agosti 26 mwaka huu wakati wa uzinduzi wa mbio za mwenge leo jijini Mbeya. Kushoto ni Kamishna wa Sensa kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Hajjat Amina Fatma Mrisho.

Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenela Mukangara (kushoto) akimtambulisha  kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda kiongozi wa mbio za mwenge mwaka 2012 Kepteni Honest Erenest Mwanossa kutoka Dar es salaam (kulia).
Kiongozi wa mbio za Mwenge Mwaka 2012, Kepteni Honest Erenest  Mwanossa kutoka Dar es salaam akikabidhi Mwenge wa Uhuru kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda tayari kwa kuukabidhi kwa viongozi wa Mkoa wa Mbeya tayari kwa kukimbizwa kwenye maeneo mbalimbali ya mkoa huo.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge Mwaka 2012, Kepteni Honest Erenest  Mwanossa (kulia) akikabidhi Mwenge wa Uhuru kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro tayari  kwa kukimbizwa kwenye maeneo mbalimbali ya mkoa huo kabla ya kuelekea mkoani Iringa

credits; mwaikenda